Ziara ya Balozi wa Tanzania Castelfranco Emilia
Na mwandishi wetu WU® MEDIA
Castelfranco Emilia, Jumamosi, 13/05/2023
Jumuiya ya Watanzania wa Centro Nord imezinduliwa rasmi leo katika sherehe kubwa iliyohudhuriwa na mgeni rasmi Balozi wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania nchini Italy Mh. Mahmoud Thabit Kombo.
Balozi wa Tanzania nchini Italy kabla ya kuhudhuria uzinduzi huo alikutana na mstahiki Meya wa jiji la Castelfranco Emilia ambako ndiko makao makuu ya jumuiya ya watanzania ya Centro Nord.
Mkutano wa Mh Balozi na mstahiki Meya ulihusu masuala ya ushirikino kati ya Mji wa Castelfranco na jiji lolote la Tanzania litakalo pendekezwa hapo baadae. Mazungumzo yao yamelenga kuunganisha pande mbili za nchi katika mahusiano ya kirafiki, elimu, utamaduni na kiuchumi. Katika kuendeleza Diplomasia ya kiuchumi, Mh Balozi amemkaribisha mstahiki Meya kuhudhuria maonesho ya kimataifa ya sabasaba yanayofanyika mwezi july, na pia Mh Balozi anategemea kurudi tena Castelfranco Emilia ili kuweza kuyajenga zaidi na mwenyeji wake Mstahiki meya wa jiji hilo Dott. Giovanni Gargano.
Baada ya mazungumzo marefu na mstahiki Meya, Balozi wa Tanzania akiongozana na Mwenyekiti wa jumuiya ya centro Nord ndugu Emmanuel B.Sanga walielekea kwenye ratiba ya ufunguzi rasmi wa jumuiya. Watanzania walikutana kwenye ukumbi wa Manispaa ya Castelfranco.
Baada ya ratiba ya utambulisho, mwenyekiti alisoma risala ya jumuiya kwa mh balozi na Kabla ya kumkaribisha mgeni rasmi, Mwenyekiti alimshukuru balozi kwa kuhudhuria uzinduzi wa jumuiya yao jambo ambalo kwao litabaki kwenye historia. Balozi alimtambulisha mama balozi Dkt. Zakia Kombo na afisa wa kitengo cha Passport na Dispora Mh. Sigfred Nnembuka ambao ameongozana nao katika hafla hiyo.
Mh. Balozi aliwapongeza Watanzania wa Centro Nord kwa hatua kubwa waliyofikia pamoja na kukamilisha usajili rasmi. Balozi kama mlezi wa Watanzania wote nchini Italy ameendelea kusisitiza umoja, upendo na ushirikiano baina ya jumuiya zote za watanzania zinazosimamiwa na kamati kuu ya diaspora.
Katika uzinduzi huo pia walihudhuria viongozi wa jumuiya ya Watanzania Italia IN CAMPANIA, Mwenyekiti (Presidente) Madame Judith Joseph, Makamu Mwenyekiti, ndugu Hussein Jiwe na Katibu wa jumuiya Dada Cecilia Lemmah. Ujumbe kutoka Jumuiya ya Watanzania Ascoli Piceno uliwakilishwa na Makamu Mwenyekiti wa jumuiya ya Muungano ndugu Dickson Lukiko nayo Kamati kuu ya diaspora Italia iliwakilishwa na makamu katibu wa kamati y a diaspora ndugu Mwinyimwaka Hatibu na Dada Halima Mwevi.