
Naibu Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Mhe. William Ole Nasha (Mb.) amekutana na kufanya mazungumzo na Spika wa Bunge la Afrika Mashariki Mhe. Martin K. Ngoga ofisini kwake jijini Dodoma tarehe 26 Januari, 2021.
Viongozi hao wamejadili namna watakavyoimarisha uhusiano baina ya Tanzania na Bunge hilo la Afrika Mashariki na kuliwezesha Bunge hilo kutekeleza majukumu yake kikamilifu huku likizingatia sheria, kanuni , taratibu na uadilifu.
Akizungumza katika kikao hicho Naibu Waziri Ole Nasha amemtaarifu Spika huyo wa Bunge la Afrika Mashariki kwamba Tanzania imekua ikifanya juhudi kubwa katika kuhakikisha nchi za Afrika ikiwemo Jumuiya ya Afrika Mashariki zinaimarisha mtangamano na kuongeza kwamba Bunge hilo la Afrika Mashariki ni moja kati ya vyombo muhimu sana katika Jumuiya ya Afrika Mashariki vinavyoimarisha mtangamano.
Amemuomba Mhe. Spika kuendelea kulisimamia Bunge hilo kwa kufuata Mkataba ulioanzisha Jumuiya ya Afrika Mashariki, Itifaki na Kanuni za Jumuiya ili kuzingatia utawala bora.








